KILIMANJARO MARATHONI 2014 YAWATEGA WAANDISHI WA HABARI.

Dk Fenella Mukangara



Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Mhe. Dk. Fenella Mukangara anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye mbio mbio za 12 za Kilimanjaro Marathon ambazo zinatarajiwa kufanyika Jumapili ijayo tarehe 2 Machi, 2014 mjini Moshi. 

Aggrey Marealle, Mkurugenzi Mkuu wa Executive Solutions, waratibu wa mbio hizo alisema jana kwamba Dr. Mukangara amekubali kuwa mgeni rasmi na atahuduria sherehe ya utoaji zawadi ambapo atatoa zawadi kwa washindi kumi wa mbio defu za kilomita 42 maarufu kama Full Marathon kwa wanaume na wanawake. 

“Uwepo wa waziri ni ishara ya uungaji mkono tukio hili na ameeleza kufurahishwa kwake na maandalizi ya hali ya juu ya Kilimanjaro Marathon. Dk. Mukangara ameeleza mara kadhaa kwamba serikali inaunga mkono Kilimanjaro Marathon kwa kutambua mchango wake michezo, utalii na uchumi,” alisema Marealle. 

Marealle aliongeza kwamba baada ya sherehe ya utoaji zawadi Waziri ataungana na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro na mpenda michezo Mhe. Leonidas Gama, wawakilishi wa wadhamini na watu wengine mashuhuri kwenye mlo maalum  wa mchana uliodhaminiwa na Kibo Palace Hotel. 

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro binafsi na kupitia ofisi yake amekuwa muungaji mkono wa Kilimanjaro Marathon na amekuwa akifurahia kukaribisha maelfu ya watu wanaokuja Moshi kutoka mataifa mbalimbali. 

Kutangazwa kwa Dk Mkangara kuwa mgeni rasmi ni kama mtego kwa waandishi wa habari za michezo kutokana na kuwepo kwa msimamo wa kutotangaza wala kuandika habari zinazomhusu Waziri huyo pamoja na Mkurugenzi wa Idara ya Habari(Maelezo), Assah Mwambene kama sehemu ya kupinga mwenendo wa serikali wa kuvifungia vyombo vya habari.

Msimamo huo ulitolewa Oktoba mwaka jana na wadau  na taasisi mbalimbali za habari ambapo katika taarifa yao walisema pia wamesikitishwa na tabia iliyoonyeshwa na Dk Mukangara na Mwambene kuchukua uamuzi wa kuyafungia magazeti ya Mwananchi na Mtanzania bila kuyasikiliza na kupotosha umma juu ya jambo hilo.

Katika hatua nyingine Mkurugenzi Mkuu wa Wild Frontiers ambao ndio waandaaji wa mbio hizo John Addison alisema “mbio za mwaka huu zimesheheeni motisha mbalimbali za kuvutia ili kuongeza idadi ya washiriki.

Washindi wa kwanza kwenye mbio ndefu za kilomita 42 (Kilimanjaro Premium Lager Marathon) wanawake kwa wanaume watajinyakulia kiasi cha shilingi milioni 4 kila mmoja, shilingi milioni mbili kwa washindi wa pili na shilingi milioni 1 kwa washindi wa tatu. 

Washindi wa kwanza kwenye mbio ndefu za  nusu marathon (km 21) wanawake kwa wanaume watajinyakulia kiasi cha shilingi milioni 2 kila mmoja, shilingi milioni 1 kwa washindi wa pili na shilingi 500,000 kwa washindi wa tatu.

Addison aliongeza kuwa medali na t-shirt zitatolewa kwa wanariadha 500 wa kwanza kumaliza mbio za kilomita 42, wanariadha 2,200 wa kwanza kumaliza mbio za nusu marathon na wanariadha 80 wa kwanza kumaliza mbio za walemavu.  Washiriki 3,000 wa kwanza kumaliza mbio za kujifurahisha za Vodacom 5km Fun Run watapewa t-shirts baada ya kumaliza mbio na watapata fursa ya kujishindia zawadi mbalimbali za kuvutia kupitia droo.

Comments

Popular posts from this blog

MAKATIBU WA CCM VUNJO WASEMA HAWANA UGOMVI NA KATIBU WAO WA WILAYA.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI, ENG. RAMO MAKANI AZINDUA MIRADI YA TANAPA CHAMWINO, DODOMA, AELEZA MIPANGO YA SERIKALI YA KUKABILIANA NA TATIZO LA WANYAMAPORI WANAOVAMIA MAKAZI YA WATU