MAPATO MANISPAA YA MOSHI "YAPAA" KUTOKA BILIONI 6.1 HADI BILIONI 9.9

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi Zuberi Kidumo akitangaza ongezeko la mapato ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi .
Mkurugenzi wa Hlamshauri ya Manispaa ya Moshi Mwajuma Nasombe akizungumza wakati wa baraza la Madiwani la Halmashauri ya Manispaa ya Moshi .
Baadhi ya Wakuu wa Divisheni na watendaji katika ofisi za Halmashauri ya Manipaa ya Moshi wakifuatilia kikao cha Bajeti cha baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo.

Baadhi ya Madiwa wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi wakichangia mjdala wa Bajeti ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi wakati wa kikao cha Bajeti .

 Na Dixon Hussein - Moshi  

Manispaa ya Moshi imepiga hatua kubwa katika ukusanyaji wa mapato ya ndani, ikiongeza mapato kutoka bilioni 6.1 mwaka 2021 hadi bilioni 9.9 mwaka 2025, ongezeko la takribani bilioni 3.7.

Mafanikio haya yanatajwa kuwa matokeo ya mikakati madhubuti iliyowekwa ili kuboresha vyanzo vya mapato na kuongeza uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali za umma.

Akizungumza katika kikao cha bajeti cha mwaka wa fedha 2025/26, Meya wa Manispaa ya Moshi Zuberi Kidumo amesema kuwa ongezeko hilo limechangiwa na mbinu mpya za ukusanyaji wa mapato pamoja na uwekezaji katika miradi yenye tija.

"Tumeimarisha mifumo yetu ya ukusanyaji wa mapato kwa kutumia teknolojia ya kisasa, tumeongeza uwazi katika makusanyo, na pia tumewekeza katika miradi inayozalisha kipato kwa manispaa. Hatua hizi zimechangia ongezeko kubwa la mapato," alisema Zuberi Kidumo .

Alisema miongoni mwa mikakati iliyochangia ongezeko la mapato ni matumizi ya Mfumo wa Kidigitali katika Ukusanyaji wa Mapato na kwamba  mifumo hiyo imepunguza upotevu wa mapato na kuongeza uwazi.

“Mfumo huu umesaidia kudhibiti mianya ya upotevu wa mapato yanayotokana na malipo ya moja kwa moja bila kufuata taratibu sahihi” alisema Kidumo

Akiwasilisha hoja kwa wajumbe wa baraza la Halmashauri ya Manispaa ya Moshi Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa hiyo Mwajuma Nasombe amesema ofisi yake kwa sasa imewekeza kwenye miradi mitatu ya kimkakatai .

Ameitaja miradi hiyo kuwa ni pamoja na ni ujenzi wa vibanda vingi vya biashara katika eneo la Uhuru Park ,Ujenzi wa bustani na kumbi za nje kwa ajili ya sherehe kwa maharusi pamoja na ukarabati mkubwa wa uwanja wa michezo wa Majengo .

Mkurugenzi Nasombe anasema Manispaa imeanzisha mfumo wa ukaguzi wa mara kwa mara kuhakikisha kuwa mapato yanayokusanywa yanafika kwenye mfuko wa manispaa bila upotevu huku usimamizi mzuri wa rasilimali na uwajibikaji wa watendaji umeimarishwa ili kuhakikisha kila senti inayokusanywa inatumika kwa maendeleo ya wananchi.

Aidha ameeleza kuwa kumekuwa na ushirikiano mzuri na  na taasisi mbalimbali za maendeleo, wafanyabiashara, na mashirika ya kimataifa katika kutafuta njia bora za kuongeza mapato na kuwekeza katika miradi mipya.

Mafanikio haya yameifanya Manispaa ya Moshi kuwa mfano wa kuigwa katika usimamizi wa fedha za umma, huku kukiwa na matumaini makubwa kuwa mapato yataendelea kuongezeka.

Hata hivyo, changamoto kama ukwepaji wa kodi na uhaba wa baadhi ya miundombinu bado zinahitaji suluhisho la haraka.

Baadhi ya wananchi wamesifu juhudi za manispaa lakini wakatoa wito wa uwazi zaidi katika matumizi ya mapato hayo.

"Tunafurahia kuona mapato yanaongezeka, lakini tunahitaji kuona miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa kasi ili wananchi waone matunda ya mapato haya," alisema mkazi mmoja wa Moshi”.alisema Idrisa Mombo mkazi wa manispaa ya Moshi

Kwa ongezeko hili la mapato, Manispaa ya Moshi inaonekana kuwa na dira thabiti ya maendeleo. Swali linalosalia ni je, mapato haya yataweza kuendelea kuongezeka kwa miaka ijayo na kubadili kabisa taswira ya kiuchumi ya manispaa?

Mwisho 

 

Comments

Popular posts from this blog

TIB YAKABIDHI MICHORO HALISI YA KITUO CHA MABASI KWA UONGOZI WA MANISPAA YA MOSHI.

MAKATIBU WA CCM VUNJO WASEMA HAWANA UGOMVI NA KATIBU WAO WA WILAYA.

BENKI KUU YATOA TAARIFA KUHUSU UPOTOSHAJI JUU YA SARAFU YA SH ,500/